Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

09 Mei 2019

UHAMIAJI YATOA ONYO KALI KWA MAWAKALA (VISHOKA) WANAOTUMIA VIBANDA VYA WAJASIRIAMALI VILIVYOPO MKABALA NA OFISI YA UHAMIAJI MAKAO MAKUU KUWATAPELI WANANCHI.

Kaimu Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Hanelore Manyanga amekutana na wafanya biashara na wajasiriamali wanaofanya biashara katika mtaa wa Loliondo, Kurasini - Jijini Dar es salaam. Mtaa huo upo Mkabala na Ofisi za Uhamiaji Makao Makuu na kuna shughuli mbalimbali za biashara ikiwamo Mamalishe, Mawakili, Wapiga picha (Passport size) pamoja na watoa huduma za Stationaries.

Kamishna Manyanga amewataka wafanya biashara hao kuisaidia Idara ya Uhamiaji kupiga vita mawakala wa huduma za Uhamiaji (Vishoka ambao wanawatapeli wananchi wanaohitaji huduma za Uhamiaji katika maeneo hayo.

“Kumekuwepo na wimbi la Matapeli wanaojifanya kuwa Maafisa Uhamiaji wanawatapeli Wananchi kwa kuchukua pesa zao na kuwaahidi kuwasaidia kupata huduma za Uhamiaji ikiwa ni pamoja na Pasipoti, Viza, na Hati za Ukaazi kwa haraka. Kupitia kikao hiki nawaagiza kuwa mfanye biashara kwa mujibu wa matakwa ya leseni zenu kama inatokea kuna mtu ambaye siyo mhusika au anatumia vibanda vyenu kuwatapeli wananchi, tafadhali toeni taarifa Uhamiaji” alisema Kamishna Hanelore Manyanga

Aidha, Kamishna Manyanga aliongeza kuwa Idara ya Uhamiaji imedhamiria kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya wale wote wanaojifanya Maafisa Uhamiaji na kuwatapeli Wananchi.
Wakitoa maoni yao katika kikao hicho baadhi ya wajasiriamali hao wametoa maoni yao na kuonesha kuchukizwa na vitendo hivyo ambavyo vinafanywa na watu ambao siyo waadilifu na kuchafua taswira nzuri ya Idara ya Uhamiaji na biashara zao kwa ujumla.

“Ni jambo jema kualikwa hapa kujadili suala hili, hata sisi tumekuwa tukichukizwa na hawa watu lakini tunashindwa kutoa taarifa kwani hatujui tumwambie nani, unakuta mtu anakuja pale mgahawani na mtu wanasaidiana kujaza fomu za Uhamiaji na baadae wanaondoka. Kupitia kikao hiki sasa tutakuwa tunatoa taarifa Uhamiaji lakini tunaomba tukitoa taarifa hizo zifanyiwe kazi na pia taarifa hizo ziwe siri” alisema Bi. Praise

Kupitia Kikao hicho wafanya biashara hao kwa pamoja wameahidi kushirikiana na Idara ya Uhamiaji na kuwafichua Mawakala/Vishoka wanaotumia Ofisi za mawakili, stationeries na migahawa kufanyia shughuli za Uhamiaji ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa yeyote atakayejihushisha na kazi za Uhamiaji katika maeneo yao ikiwa ni pamoja kufikishwa Mahakamani.

Kwa upande wake Kamishna wa Uhamiaji, Uraia na Pasipoti Gerald J. Kihinga, ametoa wito kwa Wananchi kuwa hakuna Uwakala katika huduma zinazotolewa na Idara ya Uhamiaji. Hivyo mtu anayeomba Pasipoti ya Tanzania au Vibali vya Ukaazi anatakiwa awasilishe maombi yake kupitia tofuti ya Idara ya Idara ya Uhamiaji ambayo ni www.immigration.go.tz

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Kamishna wa Uhamiaji, Uraia na Pasipoti Gerald J. Kihinga, Kaimu Kamishna wa Usimamizi na Udhibiti wa Mipaka, Naibu Kamishna wa Uhamiaji, Paul Eranga pamoja na Mkuu wa Kitengo cha Uratibu, Mrakibu Mwandamizi wa Uhamiaji Peter G. Mbaku.

Bi. Praise akichangia hoja katika kikao hicho.


Bw. Mulokozi ambaye ni mjasiriamali katika moja ya vibanda vilivyo mkabala na Ofisi ya Uhamiaji akieleza utayari wake katika kukabiliana na tatizo la vishoka wakati wa kikao hicho






Kaimu Kamishna wa Usimaizi na Udhibiti wa Mipaka, naibu Kamishna Paul Eranga akiongea wakati wa kikao hicho


Kaimu Kamishna wa Uhamiaji, Kamishna Hannelore Manyanga akiongea wakati wa kikao hicho

Baadhi wa wafanyabiasha na wajasiriamali wanaofanya shughuli zao mkabala na jengo la Uhamiaji Makao Makuu Kurasini wakiwa katika kikao cha pamoja na Idara ya Uhamiaji ili kutafuta suluhu la Vishoka wanaotumia sehemu zao za biashara kama ofisi


Kamishna wa Uraia na Pasipoti, Kamishna Gerald Kihinga akiongea wakati wa kikao hicho


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni