Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

06 Aprili 2019

TANZANIA, ETHIOPIA NA KENYA ZAKUTANA KUTAFUTA SULUHISHO LA KUTATUA TATIZO LA WAHAMIAJI HARAMU NA KUIMARISHA USHIRIKIANO MIPAKANI


Tanzania imekuwa mwenyeji wa Mkutano wa  Ngazi ya juu wa Kikanda uliofanyika katika Hotel ya Serena, Dar es Salaam kuanzia tarehe 02-04 April mwaka huu.

Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi waandamizi kutoka nchi za Tanzania, Kenya, Ethiopia, Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) na Wadau wa Maendeleo (Development Partners) ambao ni Balozi za Uingereza, Marekani, Ujerumani, Norway, Ubelgiji, EU, UN-RCO, na ICRC na kufunguliwa na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Kangi Alphaxad Lugola ulilenga  kutafuta njia ya namna ya kukabiliana na ongezeko la wahamiaji haramu, wanaoingia kinyume cha sheria hapa nchini kupitia njia ya Kusini (Southern route).

Mkutano huo ulitanguliwa na mkutano wa  Wataalamu wa masuala ya uhamiaji kutoka nchi za Tanzania, Ethiopia na Kenya chini ya Uenyekiti wa Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Peter Makakala.

Pamoja na mambo mengine nchi hizo zimeweka mikakati ya pamoja katika kushughulikia changamoto ya biashara haramu ya  binadamu (Human Trafficking & Smuggling) na usafirishaji kimagendo wa binadamu (Human Smuggling), kuangalia namna bora ya kubadilishana taarifa za Wasafirishaji (Traffickers & Smugglers) na mikakati ya kuwaondosha nchini wahamiaji haramu na kuhakikisha hawarejei tena nchini bila kufuata taratibu.

“Ni mkutano wenye nia njema kwa nchi yetu, kwani hapa tumekutana ili kuweka mikakati namna ya kudhibiti mfumo mzima wa biashara haramu ya binadamu na usafirishaji magendo ya binadamu kutoka pembe ya Afrika kupitia njia ya Kusini ambapo Tanzania ni sehemu ya hiyo njia. Majadiliano yameenda vyema na tutegemee matokeo mazuri. Kila nchi mwalikwa imeahidi kufanya juhudi katika kudhibiti tatizo hili” Alieleza Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Makakala.

Tanzania imekuwa ni njia ya Usafirishaji wa Magendo ya Binadamu kuelekea kusini mwa Afrika ambapo Idara ya Uhamiaji nchini kwa kipindi cha mwezi Januari hadi Disemba 2018 ilifanikiwa kuwamata na kuwachukulia hatua mbalimbali jumla ya wahamiaji haramu  1024 kutoka pembe ya Afrika wengi wao wakiwa raia wa Ethiopia.

Hatua mbalimbali za kudhibiti tatizo hili zimeendelea kuchukuliwa, tayari jumla ya wahamiaji haramu 583 kutoka Ethiopia waliomaliza adhabu ya kutumikia vifungo katika magereza mbalimbali nchini walirejeshwa nchini kwao katika kipindi cha mwaka jana.

Aidha katika kipindi hicho, vyombo vya usafiri 10 vilitaifishwa na Serikali baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kusafirisha wahamiaji haramu  kinyume cha Sheria za Uhamiaji.

“Tunaishia kuwakamata dereva wa Fuso anaepakia wahamiaji haramu, Tunataka madalali wenyewe wasakwe wakamatwe, Kwahiyo Kamishna Jenerali wa Uhamiaji ndani ya mwezi mmoja angalau basi kwa uchache uje na orodha ya hawa madalali wawili watatu hata kama ntaambiwa kwamba  wako nchi nyingine ili tuweze kutumia sheria zilizopo kuweza kuwakamata na kuwarejesha nchini ili kumaliza huo mtandao” Aliagiza Waziri wa Mambo ya ndani ya Nchi, Mheshimiwa Kangi Lugola.

Mkutano huu unategemea kuleta matokea chanya kwa Idara ya Uhamiaji katika suala zima la udhibiti wa wahamiaji haramu kwani ni wa kwanza kufanyika na kuwashirikisha wadau kutoka nchi za pembe ya Afrika ambako ndiko wahamiajii haramu wengi wanaokamatwa nchini hutokea pamoja na Washirika wa Maendeleo.