Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

09 Machi 2025

MAENDELEO YA WANAWAKE, MAADILI NA UCHAGUZI MKUU - AJENDA MUHIMU SIKU YA WANAWAKE JIJINI ARUSHA 2025

Na. Joseph Katonga - Arusha

Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, ambaye ndiye Mgeni rasmi katika Siku ya Kimataifa ya Wanawake nchini, amesisitiza umuhimu wa mshikamano na usawa wa kijinsia katika kufanikisha maendeleo kwa kila mmoja na taifa kwa ujumla.

Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyasema hayo kwa maelfu ya wananchi walioudhuria maadhimisho ya kitaifa ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika leo tarehe 08 Machi 2025, katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Mkoani Arusha.

Akizungumza na wananchi waliohudhuria, alisema:

"Mmedhihirisha kwamba wanawake ni jeshi kubwa na la kuaminiwa, pia niwashukuru wanaume wote waliopo hapa, wamekuwa nasi wiki nzima ya maandalizi kuelekea kilele cha siku hii ya Wanawake. Tunawashukuru sana kwa kutushika mkono."

Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alieleza kuwa hatua nyingi za kisera na kisheria zimechukuliwa na zinaendelea kuboreshwa ili kuhakikisha wanawake wanapata nafasi kubwa katika jamii na kwenye maamuzi.

Aidha, alirejea maazimio ya Mkutano Mkuu wa Beijing wa mwaka 1995, ambapo mataifa yaliweka malengo ya kufanikisha usawa wa kijinsia. Tanzania imefanikiwa kupiga hatua katika:

Kupunguza umasikini

Kupunguza na kuondoa njaa

Kuboresha sekta ya afya

Kuboresha elimu na nafasi ya wanawake katika jamii

Kuhakikisha kunakuwa na usawa wa kijinsia

Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassani aligusia pia suala zima maadili na kuwaasa wananchi wote waliohudhuria sherehe kuwa ni wajibu wa kila mzazi kuhakikisha anakuwa na maono ya jamii iliyo bora na iliyojengeka kwa msingi imara wa kimaadili, maadili yaliyomema na yatakayochochea ushirikiano miongoni mwa watu, alihimiza kwa kusema kuwa suala la maadili sio suala la serikali pekee bali ni suala la kila mmoja wetu, taasisi binafsi, taasisi za kidini nk.

Akihitimisha hotuba yake, Mhe. Dkt. Samia alizungumzia Umuhimu wa Uchaguzi Mkuu wa 2025, akiwataka wanawake kuwa mstari wa mbele kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura na kushiriki kikamilifu kwa amani na utulivu.

Maadhimisho haya ya Siku ya Wanawake Duniani 2025 yamefanyika kitaifa Mkoani Arusha, yakiwa ni chachu ya kuwapa wanawake nafasi katika sekta mbalimbali za maendeleo. Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna P. Makakala, aliongoza wanawake wa Idara ya Uhamiaji kushiriki katika maadhimisho hayo, yaliyobebwa na kauli mbiu:

"Wasichana na Wanawake 2025: Tuimarishe Haki, Usawa na Uwezeshaji."



Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna P. Makakala akiondoka uwanjani baada ya kumalizika kwa sherehe za Siku ya Wanawake Uwanja wa Amri Abeid, Jijini Arusha






Wanawake kutoka Idara ya Uhamiaji wakipita mbele ya Jukwaa kuu wakati wa Maandamano Siku ya Wanawake Duniani, Jijini Arusha



Maelfu ya wananchi wakifuatilia matukio Siku ya Wanawake Jijini Arusha

#UhamiajiUsalamaNaMaendeleo🇹🇿 #MjueJiraniYako🇹🇿 #Wanawake2025 #UsawaNaUwezeshaji


03 Machi 2025

KAMISHNA WA UHAMIAJI ZANZIBAR AFUNGA MAFUNZO YA UONGOZI NAMBA 06 YA MWAKA 2024/2025.


 #UhamiajiUpDates 

Na. Konstebo Jafar Mshihiri, Mkinga Tanga.


Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar, (CI) Hassan Ali Hassan, jana tarehe 02 Machi 2025, akiwa mgeni rasmi, amefunga rasmi mafunzo ya Uongozi kwa Maafisa na Askari wa Uhamiaji 320 katika Chuo cha Uhamiaji cha Raphael Kubaga kilichopo Wilayani Mkinga, Mkoani Tanga, Mafunzo haya ni sehemu ya kozi namba 06 ya mwaka 2024/2025.

Katika hotuba yake, CI Hassan Ali Hassan aliwapongeza Maafisa na Askari waliohitimu mafunzo yao na kuwaasa kufanya kazi kwa weledi na kuzingatia majukumu ya Idara ya Uhamiaji ili kukuza nyanja mbalimbali za kiuchumi na usalama nchini. 

"Nyinyi ni nguzo muhimu katika utendaji kazi wa Idara ya Uhamiaji, hivyo ni lazima kuonesha ufanisi, uadilifu na weledi mkubwa kwa ustawi wa usalama wa mipaka ya Nchi yetu,” alisema Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar CI Hassan A. Hassan.

Vilevile, Kamishna Hassan A. Hassan aliipongeza Brass Band ya Uhamiaji, ambayo kwa mara ya kwanza iliongoza Gwaride katika hafla ya kufunga mafunzo hayo.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo Cha Uhamiaji Raphael Kubaga Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhamiaji (SACI) Charles Obado ameishukuru serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu kwa kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya Mafunzo ya Promosheni Kozi kwa Maafisa na Askari sanjari na kutoa fedha za miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo utekelezaji wa mradi wa nyumba 12 za makazi ya wakufunzi  ambao unaendelea chuoni hapo na ukikamilika utaenda kusaidia kuboresha makazi ya wakufunzi pamoja na familiya zao kwa faida ya sasa na baadae.

Aidha amemshukuru pia Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Tanzania Dkt. Anna Makakala kwa uongozi wake uliotukuka, kwani maelekezo yake na maono yake juu ya chuo hicho yanapelekea mafanikio makubwa ya Idara ya Uhamiaji na Tanzania kwa ujumla.

Mafunzo hayo yaliyojumuisha Maafisa na Askari 320 kutoka Tanzania bara na Zanzibar yalifunguliwa rasmi tarehe 14 Desemba 2024 na kuhitimishwa Jana tarehe 02 Machi 2025 huku yakilenga kuboresha uongozi na utendaji kazi katika Idara ya Uhamiaji na Taifa kwa ujumla.




Kikundi cha Bendera

01 Machi 2025

AFISA UHAMIAJI MKOA WA MBEYA AONGOZA MAZISHI YA MRAKIBU MWANDAMIZI WA UHAMIAJI (SSI) AMON OSCAR MOGHA

 #UhamiajiUpDates Na. Konstebo Robert Ngowi, Tukuyu-Mbeya.


Afisa Uhamiaji Mkoa wa Mbeya, Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji (ACI) Filbert Ndege, kwa niaba ya Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Makakala ameongoza Mazishi ya Mrakibu Mwandamizi wa Uhamiaji (SSI) Amon Oscar Mogha, ambayo yamefanyika leo tarehe 01/03/2025, katika Kijiji cha Kayuki, Tukuyu, Wilaya ya Rungwe, Mkoani Mbeya.

Mrakibu Mwandamizi wa Uhamiaji Amon Mogha alikuwa Afisa utumishi katika Makao Makuu ya Idara ya Uhamiaji, Dodoma, alifikwa na umauti ghafla jioni ya tarehe 25/02/2025, maeneo ya Chidachi, Jijini Dodoma, akiwa njiani anatoka mazoezini.

Aidha, mwili wake uliagwa Jana tarehe 28 Februari 2025 Jijini Dodoma na kusafirishwa hadi nyumbani kwao Kijiji cha Kayuki, Tukuyu Wilayani Rungwe Mkoani Mbeya ambapo amezikwa kwa heshima na Maafisa na Askari wa Uhamiaji, familia, ndugu, na jamaa.