Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

15 Februari 2019

KAMISHNA JENERALI WA UHAMIAJI AKAGUA VIPENYO VINAVYOTUMIWA NA WAHAMIAJI HARAMU KATIKA WILAYA YA BAGAMOYO



Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Peter Makakala amefanya ziara ya kikazi katika Mkoa wa Pwani kwa lengo la kutambua vipenyo vinavyotumiwa na wahamiaji haramu kuingia hapa nchini. Akiwa katika Mkoa wa Pwani, amefanya mazungumzo na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Pwani, Mhe. Mhandisi, Evarist Ndikilo ambaye alimueleza kwamba wamejipanga katika kupambana na wahamiaji haramu katika Mkoa huo.

"Kuna mtandao mkubwa nchi nzima ambao unajihusisha na biashara haramu ya usafirishaji na magendo ya binadamu, hivyo basi hatuna budi kuvishirikisha vyombo vyetu vyote vya ulinzi na usalama katika kuhakikisha kuwa wale wote wanaojihusisha na vitendo hivi viovu wanasakwa na kushughulikiwa kwa mujibu wa sharia,” alisema Mhe. Ndikilo.

Aidha, katika taarifa yake, Mhe. Ndikilo alieleza kuwa Mkoa wa Pwani una urefu wa zaidi ya Kilometa 1300 katika mwambao wa bahari na una bandari bubu 39 zinazotumika na wahamiaji haramu kuingia nchini.

Pia Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, ametembelea Wilaya ya Bagamoyo na kukutana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ambapo, Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Zainabu Kawawa   alimueleza kuwa Wilaya hiyo ina jumla ya Vipenyo 19, pamoja na pori kubwa la Ruvu ambalo hutumiwa na wahamiaji haramu kuingia nchini.

Mhe. Mkuu wa Wilaya alivitaja baadhi ya vipenyo vinavyotumiwa na wahamiaji haramu kuingia nchini kuwa ni pamoja na Kaole, Mbegani, Mlingotini, Changwahela, Gwaza na Kondo. Hata hivyo, alimueleza kuwa, Kamati ya Ulinzi na Usalama imejipanga kufanya doria na misako maalum (special operations) za mara kwa mara ili kukabiliana na uhalifu katika katika maeneo hayo.

Aidha, Kamishna Jenerali wa Uhamiaji aliishukuru Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya Bagamoyo kwa ushirikiano wanaouonesha kwa Idara ya Uhamiaji katika kupambana na kudhibiti wahamiaji haramu nchini.

Akizungumza na Wananchi katika Kijiji cha Ruvu Darajani, Kata ya Bigwaza, Kamishna Jenerali wa Uhamiaji amewataka wananchi kutoa taarifa za uwepo wa wahamiaji haramu kwenye maeneo yao na kuacha tabia ya kuwahifadhi wahamiaji hao; kwani kufanya hivyo ni kosa kisheria na huhatarisha amani na usalama wa nchi yetu. Pia amewataka wnanchi kuwa makini na wahamiaji haramu kwani baadhi yao wanatoka kwenye nchi zenye machafuko hivyo, inawezekana wakawa wamekimbia na silaha.

“Napenda kutoa wito kwa Madereva wa vyombo vya moto kama vile magari binafsi, mabasi ya abiria, malori pamoja na bodaboda waache kuwasafirisha wahamiaji haramu, vitendo hivyo ni kosa kwa Mujibu wa Sheria ya Uhamiaji Sura ya 54, Rejeo la Mwaka 2016 pamoja na Kanuni zake. Ukithibitika kutenda makosa hayo adhabu yake ni Kifungo cha Miaka ishirini (20) au kulipa faini isiyozidi Shilingi Milioni ishirini (20) au vyote kwa pamoja,” alisisitiza Kamishna Jenerali wa Uhamiaji.

Pia Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, aliwataka Watumishi wa Idara ya Uhamiaji pamoja na Maafisa na askari wanaoshiriki katika misako na doria za wahamiaji haramu kufanya kazi kwa weledi na bidii na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma.

Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Peter Makakala akiwa na baadhi ya wajumbe Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Pwani wakati akielekea katika moja ya Bandari bubu - Bagamoyo a kuakagua Vipenyo vinavyotumiwa na wahamiaji haramu kuingia nchini

Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Peter Makakala akiwa na Mwenyeji wake Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Mhe. Zainabu Kawawa wakati alipomtembelea Ofisini kwake Bagamoyo

Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Peter Makakala akizungumza na Wazee wenyeji katika moja ya maeneo yanayopitisha Wahamiaji haramu

Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Peter Makakala akizungumza na Wananchi wa Kijiji cha Ruvu Darajani, Kata ya Bigwaza, Wilayani Bagamoyo.

















Hakuna maoni:

Chapisha Maoni