Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

26 Novemba 2019

RAIS MAGUFULI AWEKA JIWE LA MSINGI KATIKA JENGO LA OFISI YA UHAMIAJI MAKAO MAKUU DODOMA








Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dkt John Pombe Joseph Magufuli ameweka jiwe la Msingi katika ujenzi wa Mradi wa Jengo la Uhamiaji Makao Makuu Dodoma.

Akizungumza katika hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi, Mhe. Rais alisema amefurahishwa na kiwango cha ubora wa jengo hilo na kuongeza kuwa, mara baada ya kukamilika ujenzi huo, Jengo hilo la Uhamiaji litaboresha mandhari ya jiji la Dodoma.

Hata hivyo, Mhe. Rais alimtaka Mshauri Mwelekezi katika Mradi huo Prof. Evaristo Liwa kwa kushirikiana na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni kupitia upya gharama za Mradi huo na kuhakikisha gharama hizo zinashuka kutoka bilioni 30 hadi kufikia chini ya bilioni 20.

Aidha, Mhe. Rais alitumia fursa hiyo kumpongeza Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt. Anna Peter Makakala kwa kazi nzuri inayofanywa na Idara hiyo hasa katika udhibiti wa Wahamiaji Haramu kwa kushirikiana na vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama.

Kwa upande mwingine, Mhe. Rais aliwataka Makamanda na Watumishi wa Idara ya Uhamiaji kuchapa kazi kazi kwa uadilifu na kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zinazowaongoza katika utekelezaji wa majukumu yao.

Akielezea maendeleo ya Mradi huo, Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt Makakala alisema, ujenzi wa Jengo hilo umefikia asilimia 20 na kuongeza kuwa kasi ya ujenzi ni nzuri. Aidha, Dkt. Makakala alimshukuru Mhe. Rais kwa misaada mbalimbali ambayo amekuwa akiitoa kwa Idara ya Uhamiaji katika kipindi cha miaka minne tangu aingie madarakani, ikiwemo kiasi cha shilingi bilioni kumi kwa ajili ya kuanza ujenzi wa jengo hilo la Uhamiaji Makao Makuu Dodoma, ambazo alizitoa wakati wa Uzinduzi wa Mradi wa Uhamiaji Mtandao mwezi Januari, mwaka 2018.


Mradi wa Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Uhamiaji Makao Makuu upo katika eneo la National Capital City jijini Dodoma, likiwa ni eneo lenye ukubwa wa mita za mraba 13,260. Mradi huo unatekelezwa na Kampuni ya Suma JKT chini ya Mshauri Mwelekezi kutoka Chuo Kikuu Ardhi. Mradi huo ulianza kutekelezwa tarehe 27 Mei, 2019 na unatarajia kukamilika ifikapo tarehe 27 Novemba, 2020.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni