Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

15 Machi 2019

HOROHORO: WAKAZI WA MAENEO YA MPAKANI WAAHIDI KUSHIRIKIANA NA IDARA YA UHAMIAJI KATIKA UDHIBTI NA USIMAMIZI WA MPAKA.

Wakazi wa vijiji vya mpakani Wilayani Mkinga wasema wako tayari kushirikiana na Idara ya Uhamiaji katika suala zima la Udhibiti na Usimamizi wa mpaka. Wamesema hayo katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Idara ya Uhamiaji kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) uliyofanyika katika Uwanja wa Horohoro Customs katika Kijiji cha Horohoro.

Akifungua mkutano huo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Horohoro Border Ndugu Mery Mery Mirio aliishukuru Idara ya Uhamiaji kwa kukutana na Wananchi ili kutoa elimu na kujadili changamoto zilizopo maeneo ya mpakani.

Awali akimkaribisha Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji Mrakibu Ally Mtanda alisema kwamba, Idara ya Uhamiaji imeamua kwa dhati kabisa kuwashirikisha Wananchi katika Suala zima la Ulinzi na Usimamizi wa Mpaka kwani wao (wananchi) ndio wanafahamu mambo yote yanayoendelea mpakani kuliko maafisa Uhamiaji.

“Ndugu wananchi, tumekuja hapa ili kutoa elimu na kuwashirikisha katika Ulinzi na Usimamizi wa Mpaka, nyinyi ndio mnaofahamu watu wanaovusha wahamiaji haramu, wanaofanya magendo ya usafirishaji binadamu na wanaoishi na kuwauzia ardhi wahamiaji haramu. Tumeamua kuja kwenu kuwapa elimu ya uraia, umuhimu wa kushirikiana na idara ya Uhamiaji katika udhibiti na usimamizi wa mpaka tukiamini kuwa ninyi ndio wenye nchi na ndio mnaotakiwa kunufaika na Haki zinazotolewa na serikali kwa raia wake pamoja na rasilimali za Taifa. Kwahiyo mnao wajibu wa kuilinda nchi yenu ili iendelee kuwa salama.” Alieleza Mtanda.

Baadhi ya wananchi waliotoa maoni walisema kwamba wako tayari kushirikiana na Idara ya Uhamiaji kuwafichua wahamiaji haramu wanaoingia nchini. “Kwa maelezo hayo aliyotoa afande, nipo tayari kushiriki katika kuilinda nchi yangu kwani leo nimefahamu madhara yanayoweza kulikumba Taifa kwa kuwahifadhi wahamiaji haramu ikiwa ni pamoja na uwepo wa migogoro ya ardhi, kuongezeka vitendo vya kihalifu, ugaidi, usafirishaji madawa ya kulevya, na kupungua kwa na nafasi za ajira na huduma za jamii.” Alisema Mzee Ally ambaye ni Mkazi wa Horohoro kijijini.

Akifunga mkutano huo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Horohoro Border, aliishukuru Idara ya Uhamiaji kwa kutoa elimu kwa wananchi na kuitaka idara hiyo kuwa na utaratibu wa kukutana na wananchi mara kwa mara kwani wananchi wana taarifa nyingi lakini wanakuwa waoga kufika ofisi za Uhamiaji.
“Kwa mkutano huu, nimeshukuru sana, wananchi hapa wameingia hamasa na uzalendo wa kuilinda nchi yao, zamani walikuwa wanaona suala la ulinzi wa mpaka ni la vyombo vya dola pekee” Alisema Mwenyekiti huyo.

Mkutano huo ulikuwa ni kuhitimisha Warsha ya Siku tatu ya Ushirikishishwaji wa Wananchi katika Ulinzi na Usimamizi wa Mipaka iliyoanza tarehe 13 Machi na kufikia tamati leo siku ya Ijumaa, Machi 15, 2019.














Hakuna maoni:

Chapisha Maoni