Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

10 Aprili 2020

#CORONAVIRUS: UHAMIAJI MKOA WA ARUSHA YAIMARISHA UDHIBITI WA MIPAKA NA VIPENYO KWA WATU WANAOINGIA NCHINI.


Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Arusha imeimarisha Udhibiti wa uingiaji wa Watu Nchini ili kujilinda na Maambukizi ya ugonjwa wa  Corona.

Wakitekeleza  Maelekezo ya Serikali kupitia Waziri wa Afya kwamba watu wote wanaoingia nchini kuwekwa Karantini kwa muda wa siku 14 kwa gharama zao, Idara ya Uhamiaji Mkoani Arusha tayari imewakamata raia wa Tanzania 131 ambao wamerejea nchini wakitokea nchini Kenya kwa kupita katika vipenye visivyo rasmi (njia za panya) katika Maeneo ya Namanga, zoezi ambalo linafanywa na Idara ya Uhamiaji kwa ushirikiano na vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama pamoja na Wataalam wa Wizara ya  Afya.

Akizungumzia namna Idara ya Uhamiaji ilivyojipanga Kuthibiti Mipaka, Afisa Uhamiaji Mkoa wa Arusha Naibu Kamishna wa Uhamiaji Abdallah Towo amethibitisha kukamatwa kwa raia hao wa Tanzania, pamoja na raia 3 wa Kenya ambao tayari wamerudishwa nchini kwao.

Akifafanua zaidi, Kamanda Towo ameeleza kuwa  Watanzania wote 131 wamewekwa Karantini katika ya  Shule ya Sekondari Namanga na kwenye Hotel maalum zilizotengwa kwa ajili ya shughuli hiyo.

Taarifa yake inaongeza kuwa, Idara ya Uhamiaji inazishikilia jumla ya pikipiki 2 (Moja yenye usajili wa Kenya na nyingine Tanzania) ambazo zimetumiwa na baadhi yao kuingia nchini.

Ameendelea kueleza kuwa baada ya kuwahoji washikiliwa hao ilibainika kuwa kati yao ni raia 11 tu ndio walikuwa na Hati za Dharura za Kusafiria za Tanzania. Aidha, wengine wamechana/kuzitupa hati zao wakati walipokuwa wanavuka Mpaka ili kukwepa kutambuliwa kwa urahisi na kukwepa kuwekwa karantini.

Akihitimisha taarifa yake, Kamanda Towo amesisitiza kuwa Watu hao wote wamewekwa Karantini kwa muda wa Siku 14 kwa gharama zao kama ilivyoamriwa na Mamlaka zinazosimamia Ulinzi na Usalama Mkoani Arusha.

Aidha, Idara ya Uhamiaji inatoa wito kwa Watanzania na Wageni wote wanaoingia nchini kupita kwenye Mipaka ambayo imeanishwa kisheria, kwani kutumia njia za panya ni kosa kwa Mujibu wa Sheria ya Uhamiaji Sura 54, Rejeo la Mwaka 2016.

Pia Idara inatoa wito kwa wananchi wanaoishi maeneo ya mipakani kushirikiana na serikali katika kipindi hiki kwa kutoa taarifa za watu wanaoingia nchini bila kufuata taratibu ili waweze kuchukuliwa hatua na kuwekwa karantini ili kuepuka kusambaa kwa virusi vya corona bila kujua chanzo chake.


Afisa Uhamiaji Mkoa wa Arusha Naibu Kamishna wa Uhamiaji Abdallah Towo 


Pikipiki zilizokamatwa zikihusishwa na uvushaji wa watu katika njia zisizo rasmi katika eneo la Namanga mkoani Arusha

Baadhi ya raia wa Tanzania waliokamatwa na Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Arusha wakiwa ndani ya ofisi ya Kituo cha Uhamiaji Namanga.

Baadhi ya raia wa Tanzania waliokamatwa na Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Arusha wakiwa ndani ya ofisi ya Kituo cha Uhamiaji Namanga.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni