Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

06 Aprili 2020

CGI Dkt. Anna Makakala Awakumbusha Maafisa, Askari na Watumishi wa Uhamiaji Kuchukua Tahadhari Dhidi ya Corona

Dar es Salaam, Tanzania
Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Makakala
Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Peter Makakala ameyasema hayo mapema leo hii alipofanya ziara ya kikazi  katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA) ikiwa na lengo la kujionea namna watumishi wa Idara ya Uhamiaji wanavyochukua hatua za kujikinga dhidi ya maradhi ya Ugonjwa hatari wa Covid19 unaosababishwa na virusi vya Corona.

Dkt. Makakala ameupongeza uongozi wa Uwanja huo kwa kushirikiana vyema na Uhamiaji katika kuhakikisha ulinzi na usalama wa eneo hilo, lakini pia kwa namna walivyojipanga kujikinga na maambukizi ya maradhi ya ugonjwa wa Covid19 wakati wa utoaji huduma za kiuhamiaji zinazoendelea kutolewa katika uwanja huo.

Aidha ameeleza kwamba, vyombo vyote vya ulinzi na usalama viko macho katika kuhakikisha mipaka yote ya nchi inalindwa ipasavyo katika kipindi hiki ambacho watu wengine wanaweza kutumia kama faida ya kuhatarisha usalama wa Taifa.

“Wapo watu wanaweza kutumia janga hili la ugonjwa wa Covid19 kuhatarisha usalama wa nchi yetu, hivyo ni muhimu kuendelea kuwa makini katika kuilinda nchi yetu na kuendeleza ulinzi madhubuti wa mipaka yetu kwa nguvu zetu zote, Alisema.

Mbali na hilo Kamishna Jenerali Dkt. Makakala ametoa wito kwa Maafisa Uhamiaji Mikoa yote na Wafawidhi wa vituo vyote vya Uhamiaji nchini kuhakikisha wanafuata taratibu zote zinazotolewa na wataalamu wa afya katika kujikinga na maradhi hayo, na pia kuhakikisha huduma za vifaa kinga zinakuwepo muda wote katika sehemu zote za kutolea huduma za kiuhamiaji kwa faida ya sasa na baadae.  
Kwa upande wake Afisa Uhamiaji Mfawidhi wa Kituo cha Uwanja wa ndege wa Kimataifa (JNIA), Naibu Kamishna wa Uhamiaji (DCI) Fredrick Kiondo amemshukuru Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Makakala kwa kuwapatia vifaa kinga mapema tu ugonjwa huo ulipoanza kuibuka na sasa vifaa hivyo vinasaidia sana Maafisa, Askari, na wananchi kwa ujumla wanaoenda kupata huduma za kiuhamiaji kujikinga na maambukizi yanayoweza kujitokeza.

Akitoa taarifa ya mwenendo wa uingiaji wa abiria kwa sasa katika uwanja huo, DCI Kiondo alieleza kwamba kwa sasa kiwango cha kupokea ndege kimeshuka sana, ambapo hapo awali walikuwa wana uwezo wa kupokea na kuhudumia ndege karibu 19 kwa siku lakini toka ugonjwa huu umeshika kasi idadi hiyo imeporomoka kwa kasi sana na kufikia ndege moja tu.

Ndege hiyo huweza kutua mara mbili au tatu kwa wiki na huja na abiria wachache sana wengi wao wakiwa ni watanzania wanaorudi nyumbani na wakifika tu wanapimwa na wataalamu wa afya kisha wanapata huduma za kiuhamiaji na baadae huchukuliwa na magari maalumu ya serikali kwa ajili ya kuwapeleka karantini ya siku 14 kwa ungalizi na vipimo zaidi kama maagizoya serikali yanavyoelekeza.

HABARI PICHA NA MATUKIO

Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Makakala akinawa mikono mara baada ya kuwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa (JNIA Terminal III) Katika ziara yake ya kikazi


Kamishna wa Uhamiaji Divisheni ya Vibali vya Ukaazi na Pasi Mary Palmer (Ndc) akinawa Mikono mara baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa (JNIA) katika ziara ya Kamishna Jenerali wa Uhamiaji aliyoifanya mapema leo hii.


Eneo linalotumiwa na wateja  mbalimbali wanaowasili katika uwanja wa ndege wa kimataifa (JNIA) kunawa mikono ikiwa ni juhudi za kujikinga na maambukizi ya Corona


 



Maofisa Uhamiaji wa kituo cha JNIA Wakijiandaa kumpokea Kamishna Jenerali wa Uhamiaji  (Kushoto) ni Msemaji Mkuu wa Uhamiaji Mrakibu Paul Mselle
 



Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Makakala akipokea maelezo  ya huduma zinavyotelewa katika kiwanja hicho kutoka kwa Mfawidhi wa Kituo hicho Naibu Kamishna wa Uhamiaji (DCI) Fredrick Kiondo




Baadhi ya kaunta zinazotoa huduma za kiuhamiaji 
Mfawidhi wa Kituo cha (JNIA ) Naibu Kamishna wa Uhamiaji (DCI) Fredrick Kiondo akitoa maelezo ya awali kuhusu shughuli zanazofanyika katika kituo anachokisimamia


Muonekano wa nje wa Jengo la Abiria Terminal III Katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa JNIA (Picha zote na Kitengo cha Uhusiano Uhamiaji Makao Makuu)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni