Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

11 Aprili 2020

#COVID-19TZ: UHAMIAJI KAGERA YATEKELEZA AGIZO LA KAMISHNA JENERALI DKT. MAKAKALA KUTHIBITI UINGIAJI HOLELA WA WATU NCHINI.

Idara ya Uhamiaji Mkoani Kagera imeanzisha progamu za Elimu kwa Umma na Ukaguzi (Doria na Misako) kwa lengo la kuimarisha udhibiti wa uingiaji wa watu nchini.

Akizungumzia Mikakati hiyo Afisa Uhamiaji Mkoa wa Kagera, Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji Upendo  Buteng’e amesema Idara ya Uhamiaji kwa ushirikiano na Vyombo vingine vya Ulinzi na Usalama Mkoani humo, wamefanya ukaguzi kwa vipenyo (Panya Road) ambavyo vinatumiwa na Watanzania na raia wa kigeni kuingia nchini kinyemela.

Kijiografia, Mkoa wa Kagera unapakana na Nchi za Burundi, Rwanda, Uganda pamoja na Uwanda Mkubwa wa Ziwa Victoria ambao unapakana na Kenya.

Kutokana na muingiliano mkubwa wa watu na uwepo wa vipenyo vingi, Uhamiaji Mkoa wa Kagera wameanzisha program maalum za Ukaguzi (Doria na Misako) na Elimu kwa Umma kwa kuwashirikisha moja kwa moja Wananchi, Madereva wa Magari ya Usafirishaji mizigo na Viongozi wa Serikali za Vijiji na Mitaa hususan maeneo ya mipakani kuacha kuwapokea Watanzania na wageni wanaoingia nchini kupitia kwenye maneo yao.

Zoezi hili limeanza tarehe 31/03/2020 ambalo litaendelea kwa muda wa siku 30 linahusisha pia ukaguzi wa vipenyo na mialo iliyopo katika Wilaya za Bukoba,  Missenyi, Kyerwa na Ngara.

Pamoja na udhibiti wa uingiaji wa watu nchini pia wananchi wametakiwa kuchukua tahadhari zote za kujikinga na ugonjwa wa Corona kwa kufuata maelekezo yanayotolewa na Serikali kupitia Wizara ya Afya ikiwa pamoja na kunawa mikono kwa maji tiririka na sabuni pamoja na vitakasa mikono na Barakoa wakati wote.

Aidha, Idara ya Uhamiaji inawataka Madereva wa magari makubwa ya mizigo kuacha kubeba abiria kwenye magari yao, endapo watabainika kufanya hivyo hawataruhusiwa kuendelea na safari zao na badala yake watawekwa Karantini kwa muda wa siku 14 kwa gharama zao wenyewe. Tofauti na ilivyo sasa kwamba wanaendelea na safari zao baada ya kufanyiwa vipimo na kuonekana wako salama.

Wakati huo huo Wananchi wengine wametakiwa kutofanya safari zozote ambazo siyo za lazima kwasababu Nchi jirani wamezika watu kuingia katika Nchi zao.

Hata hivyo Idara ya Uhamiaji inatoa wito kwa wananchi wasiokuwa na  safari za lazima waahirishe safari zao hadi hapo hali itakapokuwa sawia.

Ikumbukwe kuwa zoezi linafanywa ikiwa ni Utekelezaji wa Agizo la Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Makakala alilotoa hivi karibuni alipokagua kituo cha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. Julius Nyerere (JNIA) ambapo kwa Mkoani Kagera linafanywa kwa ushiriano na Vyombo vya Ulinzi na Usalama Mkoa pamoja na Wilaya za Bukoba, Missenyi, Kyerwa na Ngara na Wataalam kutoka Wizara ya Afya

Afisa Uhamiaji Mkoa wa Kagera, Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji Pendo  Buteng’e akitoa taarifa ya utekelezaji wa agizo la Kamishna Jenerali wa Uhamiaji katika Ofisi ya Uhamiaji Mkoa Kagera mjini Bukoba 

Kituo cha Uhamiaji Mutukula kilichopo mpakani mwa Tanzania na Uganda kinachohudumia raia na wageni wanaokwenda nchi za Uganda, Sudani Kusini na DRC

Afisa Uhamiaji Mkoa wa Kagera, Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji Pendo  Buteng’e akiwa wilayani Kyerwa katika utekelezaji wa agizo la kumarisha doria na misako mkoani Kagera. 

Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Kagera, wakiongea na wananchi walipotembelea kijiji cha mpakani cha Rubafu.

Ukaguzi wa 'njia za panya' katika kijiji cha mpakani cha Kakoni wilayani Kyerwa uliofanywa na Idara ya Uhamiaji mkoa wa Kagera kwa ushirikiano na vyombo vingine vya dola mkoani humo.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni