Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

15 Aprili 2020

#COVID-19 Uhamiaji Rukwa Kupambana na Vipenyo Haramu Kudhibiti Corona

Rukwa, Tanzania
Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Leonard Wangabo akiambatana na Afisa Uhamiaji Mkoa, Naibu Kamishna wa Uhamiaji DCI Elizeus Mushongi na Mganga Mkuu wa Mkoa, wamefanya ziara ya  ukaguzi wa vipenyo haramu katika Wilaya ya Nkasi Mkoani humo, ikiwa ni utekelezaji wa kupambana na kudhibiti maambukizi ya Ugonjwa wa COVID-19 unaosababishwa na Virusi vya Corona.

Katika ziara hiyo elimu ya sheria za Uhamiaji na jinsi ya kujikinga na maambukizi ya ugonjwa wa COVID-19 ilitolewa katika vituo vya Kabwe, Kirando na Wampembe kwa kuongea na Watendaji wa Kata na vijiji, madiwani, wenyeviti wa vijiji na vitongoji.

Ziara hiyo ilihitimishwa Jumapili ya pasaka kwa kusali na kuongea na waumini wa Kanisa Katoliki Parokia ya Namanyere, wilayani Nkasi, ambapo pia walipata fursa ya kutoa elimu kwa waumini.

Mhe. Wangabo alitoa wito kwa wananchi wa Mkoa huo kuhakikisha wanafuata ushauri unaotolewa na wataalamu wa Afya na kutopokea wageni wanaoweza kuingia nchini kinyume na sheria, sanjari na kuhakikisha boti zote zinazoingia katika mwambao mwa ziwa Tanganyika kupitia katika vituo vilivyo rasmi, ili kufanyiwa vipimo hali itakayopunguza maambukizi virusi vya Corona.

Akitoa taarifa fupi ya ziara hiyo Afisa Uhamiaji Mkoa wa Rukwa DCI Mushongi alieleza kwamba takribani watu 45 waliotoka nje ya nchi kupitia mpaka wa mwambao wa Ziwa Tanganyika wamewekwa karantini Mkoani humo baada ya kumaliza taratibu za kiuhamiaji, ambapo Kirando katika ziwa Tanganyika ina idadi ya watu 22, Kabwe 17, Kasesya 03, na Sumbawanga Mjini 03.

Zoezi hilo la kuwaweka karantini wageni na raia wa Tanzania wanaoingia hapa nchini kupitia mipaka mbalimbali ni utekelezaji wa maelekezo ya serikali kwa wananchi na wageni wanaongia  nchini kujitenga kwa siku 14 kwa kujitegemea.
Raia hao na wageni walioingia nchini hivi karibuni mpaka sasa wako chini ya uangalizi wa wataalamu wa Afya kwa ajili ya kuafanyiwa vipimo kuhusu hali zao za kiafya.

Aidha katika idadi hiyo ya waliowekwa karantini watanzania ni 40, raia wa Congo 04 na raia 01 mwenye asili ya Omani.

Jeshi la Uhamiaji chini ya Kamishna Jenerali Dkt. Anna Makala linaendelea kuwa hodari na shupavu katika kutimiza majukumu yake ya msingi katika kulinda mipaka ya nchi na kuendesha doria za mara kwa mara katika mipaka yote na kudhibiti vipenyo vinavyosadikika kupitisha wahamiaji haramu ili kulinda Amani na Usalama wa nchi yetu.

HABARI PICHA NA MATUKIO
Naibu Kamishna wa Uhamiaji Elizeus Mushongi akitoa elimu ya sheria za uhamiaji kwa Watendaji wa Kata na vijiji, madiwani, wenyeviti wa vijiji na vitongoji (hawapo pichani)

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (katikati) akiwa na Naibu Kamishna wa Uhamiaji Mkoa (kushoto),  katika ibada ya pasaka iliyofanyika katika kanisa Katoliki Parokia ya Namanyere

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni