Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

05 Machi 2021

Uhamiaji Zanzibar yatoa mafunzo ya E-visa kwa wadau wa utalii na kampuni za usafirishaji

Zanzibar



Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar, Johari Masoud Sururu ameongoza  semina ya viza za kielektroniki kwa wadau mbali mbali wa utalii na kampuni za usafirishaji (ground handler) mapema mwaka huu katika ukumbi wa mkutano wa Afisi Kuu ya Uhamiaji Zanzibar.

Katika mkutano huo amewashajihisha wadau juu ya matumizi ya e-visa, badala ya kuomba visa wakati mgeni akiingia nchini (visa on arrival) ambayo inaombwa wakati mgeni anapowasili kupitia vituo vya kuingilia nchini ambapo imekuwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuleta usumbufu kwa wageni, kwani hulazimika kujaza fomu ya maombi ya viza baadae kuwasilisha katika kaunta za Uhamiaji, kufanyiwa mahojiano, kupatiwa control namba kwa ajili ya malipo, kwenda benki kufanya malipo na kurudi tena katika kaunta za Uhamiaji kwa kupata ruhusa husika ya kuingia nchini. 

Ni utaratibu wa kisheria na kifedha lakini hata hivyo umeonekana kuleta usumbufu kidogo kwa wageni wanaoingia hapa nchini. 

Kwa upande wake mkuu wa kitengo cha TEHAMA Uhamiaji Zanzibar Mrakibu Msaidizi wa Uhamiaji Muhsin Ali Masheko amezidi kuwahamasisha wageni kuomba viza  kwenye mtandao badala ya kuomba  wakati wa kuingia nchini, sanjari na kuwaelezea athari za kuomba viza wakati wa kuwasili nchini, pia  ameeleza kuhusu pasipoti za  kikimbizi na kuwataka wadau hao kuitambua pasipoti hiyo ya kikimbizi (convention passport) ambayo hutumiwa na wageni wasiokuwa raia halisi wa nchi husika. 

Aidha, mkuu huyo wa kitengo cha TEHAMA ameongeza kuwashajihisha wageni kujaza fomu za kuingilia nchini (TIF. 10) wakiwa nyumbani kabla ya kuingia nchini inayopatikana baada ya ombi kukubaliwa badala ya kusubiri kujaza kwenye ndege au wakiwa vituoni wanapoingia kwa ajili ya kupunguza muda wa kukaa katika kaunta za kupokelea wageni.

HABARI PICHA NA MATUKIO

Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar, Johari Masoud Sururu akiongoza  semina ya viza za kielektroniki kwa wadau mbali mbali wa utalii na kampuni za usafirishaji (ground handler)


  Wadau mbali mbali wa utalii na kampuni za usafirishaji wakifuatilia kwa makini semina ya viza za kielektroniki iliyotolewa na Idara ya Uhamiaji Zanzibar

 Mkuu wa Kitengo cha TEHAMA Uhamiaji Zanzibar Mrakibu Msaidizi wa Uhamiaji Muhsin Ali Masheko akitoa ufafanuzi juu ya huduma za e-Visa




(Picha zote na Kitengo cha Uhusiano Uhamiaji Zanzibar)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni