Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

23 Novemba 2017

KAMISHNA WA UHAMIAJI ZANZIBAR AFANYA ZIARA MKOA WA KUSINI UNGUJA

Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar, Johari Masoud Sururu, amefanya ziara ya kikazi katika Mkoa wa Kusini Unguja ikiwa ni utaratibu wa kawaida kutembelea vituo na ofisi za uhamiaji Zanzibar.

Ziara hiyo iliyokuwa na malengo makuu mawili, Kwanza ni kukagua miradi mbalimbali na viwanja vilivyopo katika Mkoa huo. Miradi ya ujenzi wa nyumba za kuishi Watumishi na ofisi ni hatua muhimu katika kutanua wigo wa utoaji huduma mbali mbali za Uhamiaji kwa Wilaya zote za Unguja na Pemba ambayo ni utekelezaji wa ahadi za Serikali kuwafikishia wananchi wake huduma katika maeneo wanayoishi.

Pili, ilikuwa ni kuhimiza askari na maafisa uhamiaji kufanya kazi kwa weledi, uaminifu na kujituma ili wananchi wapate huduma kwa wakati.

Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji Khamis Ali Juma kutoka katika ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Kusini Unguja alimweleza Kamishna maendeleo ya miradi ya ujenzi wa nyumba za makazi ya watumishi na ofisi katika mkoa huo pamoja na namna walivyojipanga kutoa huduma kwa weledi.

Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar Johari Masoud Sururu, alieleza jinsi Idara ya Uhamiaji inavyopiga hatua katika ujenzi wa Makazi ya Askari wake katika Wilaya zote Unguja na Pemba.

"Nimekuja kukagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba za makazi ya Watumishi hapa Makunduchi, Wilaya ya Kusini. Ujenzi unaendelea vizuri, tunategemea zikikamilika zitapunguza tatizo la upungufu wa nyumba za makazi ya watumishi. Tunavyo viwanja katika mkoa huu, tunategemea kununua viwanja vingine kwa ajili ya miradi hapo baadae.” Alieleza Kamishna wa Uhamiaji huyo.

Ziara hiyo ya siku mbili katika Mkoa wa Kusini Unguja imekuwa na mafanikio kwa kiasi kikubwa kwani kero mbalimbali zilipatiwa majibu ya kuridhisha pamoja na miradi iliyokaguliwa kubainika kuwa inakwenda vizuri. Kamishna Uhamiaji wa Zanzibar pamoja na majukumu mengine amekuwa akitembelea Ofisi na Vituo vya Uhamiaji Unguja na Pemba kuhimiza utendaji kazi unaofuta misingi na sheria. 


Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar Johari Masoud Sururu akisisitiza jambo wakati wa kikao na watumishi wa Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Kusini Unguja

Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar Johari Sururu akisaini kitabu cha wageni katika ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Kusini wakati ya ziara yake katika mkoa huo.

Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar akitoa maelekezo wakati wa ukaguzi wa nyumba za makazi ya watumishi zinazohitaji ukarabati.


Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji Khamis Ali Juma kutoka katika ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Kusini Unguja akimweleza Kamishna wa Uhamiaji juu ya maendeleo ya miradi ya ujenzi wa nyumba za makazi ya watumishi na ofisi katika mkoa huo.


Maafisa waandamizi wa Idara ya Uhamiaji Zanzibar, wakiambatana na Kamishna wa Uhamiaji Zanzibar, Johari Masoud Sururu (katikati), wakati alipofanya ziara ya kikazi Wilaya ya Kati na Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja. Hapa ilikuwa ni ukaguzi Viwanja vilivyopo Mkoani wa Kusini Unguja.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni