Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

08 Januari 2020

Zaidi ya Watanzania 230,000 wapatiwa Pasipoti Mpya za Kielekroniki

Idara ya Uhamiaji Tanzania kwa kipindi cha Januari 2018 mpaka Disemba 2019 imetoa zaidi ya pasipoti mpya za kielekroniki 230,000 kwa raia wa Tanzania.

Hayo yamesemwa mapema leo hii na Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji Tanzania Mrakibu Mwandamizi wa Uhamiaji, Alhaj Ally Mtanda wakati akiongea na waandishi wa habari katika Ofisi za Uhamiaji Kurasini, Jijini - Dar es salaam.

“Tulitoa miaka miwili kwamba itakapofika tarehe 31 Januari 2020 tutasitisha matumizi ya huduma za pasipoti za zamani yaani (MRP) tulianza huduma hii ya utoaji pasipoti mpya  za kielekroniki kwa ofisi za makao makuu ya Uhamiaji Tanzania bara na Afisi Kuu ya Uhamiaji Zanzibar, lakini mpaka sasa huduma hii tumeisogeza katika Mikoa yote hapa nchini na katika Balozi zetu zote za nje ya nchi ili kuwasaidia Watanzania kubadilisha pasipoti zao, kupata Pasipoti  mpya na huduma nyingine za kiuhamiaji kwa urahisi kwa kutumia njia ya mtandao” alisema Mtanda.

Kwa ujumla kumekuwa na mwitikio mkubwa kwa Wananchi kujitokeza kubadilisha pasipoti zao pamoja na waombaji wapya wa pasipoti za kielektroniki, ambapo takwimu zinaonesha kwa kipindi cha tarehe 31 Januari 2018 hadi 31 Disemba 2019 takribani Watanzania 239,946 waliweza kukidhi vigezo vya kupatiwa pasipoti, kwa mujibu wa sheria ya Pasipoti na hati za safari Sura ya 42 ya Mwaka 2002 na Kanuni zake za Mwaka 2004.

Mchanganuo wa Pasipoti zilizotolewa kwa kipindi hiki ni kama ifuatavyo, pasipoti za kawaida yaani (Ordinary Passport) 237,813 zimetolewa kwa wananchi, pasipoti za utumishi (Service Passport) kwa viongozi waandamizi wa serikali idadi 459 na pasipoti za kidiplomasia (Diplomatic Passport) ambazo wanapewa viongozi wanye hadhi ya kidiplomasia wakiwemo mawaziri, mabalozi  na wabunge  idadi ni 1672 na pasipoti maalumu za kidiplomasia zilizotolewa kwa viongozi wa juu wa Serikali 05 hivyo kuleta idadi ya jumla ya pasipoti 239,946.

Ikumbukwe kuwa zoezi la ubadilishaji wa pasipoti za zamani (MRP) kuelekea pasipoti mpya za kielektroniki lilizinduliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 31 Januari mwaka 2018, katika Ofisi za iliyokuwa Makao Makuu ya Uhamiaji, kurasini, Jijini Dar es Salaam, ili kuendelea kukidhi utoaji wa huduma za kiuhamiaji kwa viwango vya kimataifa.

Aidha gharama zote za upatikanaji wa pasipoti hii mpya ya kusafiria ya kielekroniki ni Tsh. 150,000 tu kwa watanzania waishio hapa nchini na kwa waishio nje ya nchi gharama yake ni dola za kimarekani 90 (USD) tu.

HABARI NA MATUKIO 
Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji Tanzania Mrakibu Mwandamizi Alhaj Ally Mtanda
Mteja akipatiwa pasipoti yake katika ofisi za Uhamiaji Kurasini Dar es salaam mara baada ya kumaliza hatua zote za uombaji 
Mmoja wa wateja waliofika katika ofisi za uhamiaji kurasini jijini Dar es salaam akifurahia pasipoti mpya ya kielekroniki kulia kwake ni Msemaji wa Idara ya Uhamiaji Tanzania Mrakibu Mwandamizi wa Uhamiaji SSI Alhaj Ally Mtanda


Mteja akionesha pasipoti yake mpya ya kielekroniki mara baada ya kumaliza hatua zote na kuipata
Uchukuaji wa Alama za vidole ikiwa ni hatua muhimu za kupata pasipoti mpya ya kielekroniki



Picha zote na Kitengo cha Uhusiano Uhamiaji Makao Makuu

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni