Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

10 Januari 2020

#TUJIKUMBUSHE Historia ya Pasipoti Mpya ya Kielektroniki Tanzania


Wakuu wa nchi wanachama wa jumuiya ya Afrika Mashariki mwezi Novemba 2013, waliamuru kila nchi mwanachama ianze mchakato wa kutoa pasipoti mpya ya Afrika Mashariki.

Tarehe 02 machi 2016 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli na waheshimiwa marais wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kilele cha mkutano wao uliofanyika Arusha Tanzania, walikubaliana rasmi kuanza kutoa pasipoti za kielekroniki (EA-eppt) ifikapo Januari 2017.

Idara ya Uhamiaji Tanzania bila kuchelewa ilitekeleza kwa vitendo agizo hilo na kuwa nchi ya kwanza kuanzisha pasipoti mpya zote za kielekroniki katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mnamo Januari 31, 2018 Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli alizindua rasmi mfumo wa utoaji huduma za uhamiaji mtandao (e-Immigration) na hivyo kuifanya Tanzania kuanza nchi ya kwanza kutoa aina zote nne za Pasipoti mpya ya kielektroniki yaani pasipoti ya kawaida, utumishi, kidiplomasia na pasipoti Maalumu za Kidiplomasia kwa wakati mmoja.

Pasipoti hii ya kisasa imekidhi viwango vya ubora vya kimataifa vinavyopendekezwa na shirika la umoja wa mataifa linalosimamia usafiri wa anga (International civil aviation organization-ICAO).

Machi, 2019 pasipoti mpya ya Kielektroniki ya Tanzania iliibuka kidedea na kupata tuzo ya ubora katika viwango vya kimataifa vya usalama na kuwa pasipoti bora katika ukanda wa Ulaya, Mashariki ya Kati, na Afrika (Europe, Middle East and Afrika - EMEA)
Katika kipengele cha utambulisho (National Identity) pasipoti hii imesanifiwa kwa kuzingatia utamaduni wa Kitanzania na maliasili tulizonazo ambazo ni fahari ya nchi yetu.

Michoro iliyopo katika pasipoti hiyo ni pamoja na wanyama, majengo ya kihistoria, matukio ya kitaifa na nukuu za hamasa za hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Kuhusu eneo la usalama, Pasipoti hii ina kifaa maalumu chenye uwezo wa kutunza taarifa za mmiliki wa pasipoti “Micro Chip” na hivyo kufanya suala la utunzaji wa usalama wa pasipoti hizi kuwa wa hali ya juu zaidi.
Pasipoti hii ina uwezo wa kutunza kumbukumbu za kibailojia (Biometric features) na alama za usalama ambazo si rahisi kwa mtu yeyeote kuzibaini hivyo kuwa vigumu kughushiwa na wahalifu au watu wanaojaribu kuficha utambulisho wao kwa kutumia pasipoti zisizo kuwa zao.

Faida za pasipoti ya kielektroniki (e-Passport) ni utambulisho wa pamoja wa raia wa nchi wanachama wa EA wanapokuwa nje na hivyo kurahisisha kupata msaada wa huduma za kikonsula (Consular Services) mfano kupata msaada wa kurejeshwa nchini kupitia balozi za nchi wanachama wakati wa dharula ikiwa sehemu husika haina ubalozi wa Tanzania.

Mbali na hilo pia husaidia wanachama kutambuana wanapokuwa nje ya nchi hivyo kujenga umoja na ushirikiano sanjari na kurahisisha utambuzi na utunzaji wa kumbukumbu za raia wa Afrika Mashariki.
Ikumbukwe kuwa utekelezaji wa mradi wa utoaji pasipoti mpya za kielektroniki ulifanyika kwa muda mfupi sana kwa ufadhiri wa serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli.

Idara ya Uhamiaji Tanzania kwa kipindi cha Januari 2018 mpaka Disemba 2019 imetoa zaidi ya pasipoti mpya za kielekroniki 230,000 kwa raia wa Tanzania waliokidhi vigezo vya kupatiwa pasipoti hizo kwa mujibu wa sheria ya pasipoti ya Tanzania ya mwaka 2002 sura ya 42 na kanuni zake za mwaka 2004.

“Tulitoa miaka miwili kwamba itakapofika tarehe 31 Januari 2020 basi tutasitisha matumizi ya huduma za pasipoti za zamani yaani (MRP) tulianza huduma hii ya utoaji pasipoti mpya za kielekroniki kwa ofisi za iliyokuwa makao makuu ya Uhamiaji Tanzania iliyopo Kurasini Jijijini Dar es salaam na Afisi kuu ya Uhamiaji Zanzibar, lakini mpaka sasa huduma hii tumeisogeza katika mikoa 29 Tanzania bara hivyo kuleta idadi ya vituo 31vya kutolea huduma hiyo, Katika balozi zetu pia za nje ya nchi ili kuwasaidia watanzania kubadilisha pasipoti zao, kupata Pasipoti mpya na kupata huduma za kiuhamiaji kwa urahisi ikiwemo kutumia njia ya uhamiaji mtandao takribani Balozi 44 zimefungwa mfumo huo” alisema SSI Alhaj Ally Mtanda Msemaji Mkuu wa Idara ya Uhamiaji Tanzania.

Kwa ujumla kumekuwa na mwitikio mkubwa kwa wananchi katika kuja kubadilisha pasipoti zao na wengine kufanya maombi ya pasipoti mpya, ambapo takwimu zinaonesha kwa kipindi cha tarehe 31 Januari 2018 hadi 31 Disemba 2019 mwaka jana takribani Watanzania 239,946 waliweza kukidhi vigezo vya kupatiwa pasipoti mpya ya kielektroniki kwa mujibu wa sheria.

Mchanganuo wa Pasipoti zilizotolewa kwa kipindi hiki ni kama ifuatavyo, pasipoti za kawaida yaani (Ordinary Passport) 237,813 zimetolewa kwa wananchi, pasipoti za utumishi (Service Passport) kwa viongozi waandamizi wa serikali idadi 459 na pasipoti za kidiplomasia (Diplomatic Passport) ambazo wanapewa viongozi wa juu wa nchi wakiwemo mawaziri, mabalozi na wabunge idadi ni 1672 na pasipoti maalumu za kidiplomasia 05 hivyo kuleta idadi ya jumla ya pasipoti 239,946.

Idara ya Uhamiaji inasisitiza na kukumbusha mwisho wa kutumia pasipoti ya zamani yaani (MRP) ni 31 Januari mwaka huu 2020, ewemwananchi epuka usumbufu usiokuwa wa lazima wahi mapema kubadili pasipoti yako.

Aidha gharama zote za upatikanaji wa pasipoti hii mpya ya kusafiria ya kielekroniki ni Tsh.150,000 tu kwa watanzania waishio hapa nchini na kwa waishio nje ya nchi gharama yake ni dola za kimarekani 90 (USD)tu.

HABARI PICHA
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akionesha pasipoti yake mpya ya kiilektroniki wakati ilipozinduliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 31 Januari, 2018 katika ofisi za Uhamiaji Kurasini Jijini Dar es salaam
Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli akitia saini pasipoti yake mpya ya kielekroniki wakati wa uzinduzi wa utoaji wa pasipoti hizo mpya kwa raia wa Tanzania
Mke wa Rais wa Tanzania Mama Janeth Mgufuli nae akipata huduma ya pasipoti mpya ya kielektroniki na hapa anachuku alama za vidole kama hatua moja wapo ya kukamilisha tartibu za upatikanaji wa Pasipoti hiyo





(Picha zote kwa hisani ya Mawasiliano Ikulu blog)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni