Visitors

IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA UHAMIAJI HABARI BLOGU KARIBU KWENYE BLOG RASMI YA IDARA YA UHAMIAJI TANZANIA TUNAKULETEA MATUKIO YANAYOTOKEA KILA SIKU KATIKA IDARA YA UHAMIAJI TAFADHALI TUNAOMBA TUFUATILIE PIA KATIKA MITANDAO YETU YA KIJAMII

05 Machi 2020

Uhamiaji na Airtel Wazindua Huduma za Malipo ya Ada ya Pasipoti kwa njia ya Airtel Money


Dar es salaam, Tanzania
Idara ya Uhamiaji Tanzania kwa kushirikiana na Kampuni ya mawasiliano ya Airtel mapema leo hii tarehe 5 Februari 2020 tumezindua huduma ya malipo ya ada za pasipoti kwa njia ya Airtel Money ili kuongeza wigo wa malipo ya huduma za pasipoti.

Mgeni rasmi wa Uzinduzi huo Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhamiaji (SACI) Mohamed Awesu ambae pia ndie Mfawidhi Mkuu wa TEHAMA Katika Jeshi la Uhamiaji Tanzania amesema Matumizi ya huduma hii yatamrahisishia mwombaji wa pasipoti kufanya malipo kutoka mahali popote alipo.

“Ili kutumia huduma hii mteja anatakiwa kutembelea tovuti ya Idara ya Uhamiaji (www.immigration.go.tz), atajaza fomu yake na baada ya kukamilisha kujaza atapatiwa Namba ya Kumbukumbu ya malipo (Control Number) ambayo ndiyo ataitumia kufanya malipo kwa njia hiyo ya Airtel Money. Baada ya hapo ataiprint na kisha kuiwasilisha fomu hiyo katika Ofisi ya Uhamiaji kwa taratibu zinazofuata” alisema.

Hatua ya kutumia huduma hii ya Airtel Money ni utekelezaji wa sera ya Serikali ya kwa taasisi zake zote kufanya malipo ya huduma mbalimbali kupitia Mfumo wa Serikali wa malipo kwa njia ya Mtandao GePG.

Mfumo huo umerahishisha sana malipo na umekuja na faida nyingi kama vile kurahisisha malipo, kuimarisha utunzaji wa kumbukumbu, kupunguza upotevu wa mapato ya Serikali, kuondoa mianya ya rushwa pamoja na kuongeza mapato ya serikali.

Aidha SACI Awesu ameipongeza Kampuni ya Airtel Tanzania kwa kuweza kuungana na Huduma za Uhamiaji kama ilivyo kwa mitandao mingine ya mawasilano hapa nchini ili kuwawezesha Watanzania kufanya malipo ya pasi za kusafiria kwa kutumia huduma ya “Airtel Money”, hatua hii inaendelea kurahisisha na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma ya Pasipoti.

Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania Bw. Isack Nchunda, amemshukuru Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. Anna Peter Makakala kwa  ushirikiano mkubwa aliouonesha wakati wote wa mchakato wa kuelekea tukio hili la ufunguzi wa huduma hii ili kuwarahisihia wananchi kupata huduma ya pasipoti kwa urahisi na kufanya malipo sehemu yoyote ile.

Bwana Nchunda aliongeza kuwa mwombaji anaweza kulipa ada yake ya maombi ya  pasipoti baada ya kupewa kumbukumbu ya malipo (Control Number) ambapo unapiga *150*60# Unachagua kufanya malipo Namba 5, Kisha unachagua malipo ya serikali, halafu unaingiza namba ya kumbukukumbu ya malipo unaweka kiasi kama ni ada ya fomu ya Pasipoti ambayo gharama yake ni Tsh 20,000tu na ada ya Pasipoti baada ya kuprinti fomu zikishakaguliwa na Maafisa Uhamiaji Unamalizia Tsh.130,000 tu ambayo huleta gharama ya pasipoti kwa Tsh. 150,000tu.

Sanjari na hilo unamalizia kwa kuingiza namba zako za siri na kisha unathibitisha malipo yako na ndani ya sekunde 10 mpaka 15 unapata ujumbe wa malipo yako kupokelewa.

Kampuni ya Mawasiliano ya Airtel Money ni Kampuni inayomilikiwa na serikali kwa asilimia 49% ndio maana inarahisisha maisha kwa kushirikiana na Uhamiaji, kuhakikisha watanzania wanapata huduma bora kupitia Airtel Money kwa haraka na uhakika zaidi.

Mfumo wa Uhamiaji Mtandao ulizinduliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt John Pombe Magufuli tarehe 31 Januari, 2018. Tangu wakati huo, fomu za maombi ya Pasipoti zimekuwa zikijazwa kwa njia ya mtandao, Hivyo Uhamiaji Tanzania inatoa wito kwa wananchi kuendelea kutumia huduma hii ya Airtel Money katika kufanya malipo yao ya ada za pasipoti kwani ni salama na rahisi kutumia.

 HABARI PICHA NA MATUKIO
Mgeni rasmi wa Uzinduzi huo Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhamiaji (SACI) Mohamed Awesu (katikati) ambae pia ndie Mfawidhi Mkuu wa TEHAMA Katika Jeshi la Uhamiaji Tanzania akipokea alama ambayo ni Ishara ya Uzinduzi wa  malipo ya Ada ya Pasipoti kwa njia ya AirtelMoney




Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji Dorah Luoga (katikati) ambae pia ndie Mdhibiti wa Pasipoti Katika Jeshi la Uhamiaji Tanzania ajitoa shukrani kwa Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania Bw. Isack Nchunda Pasipo kupeana mikono ikiwa ni Utekelezaji wa Ushauri wa Waziri wa Afya, hapa ni katika uzinduzi wa  malipo ya Ada ya Pasipoti kwa njia ya AirtelMoney katika Ofisi Ndogo za Uhamiaji Makao Makuu Kurasini Dar es salaam
Huduma zikiendelea kutolewa kwa wateja kujua namna ya kulipia pasipoti kwa njia ya Airtel Money




Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania Bw. Isack Nchunda akitoa maelezo mafupi ya namna ya kufanya malipo ya ada ya pasipoti kwa njia ya Airtel Money

Afisa Uhusiano Mrakibu Msaidizi akiongoza itifaki katika tukio zima la Uzinduzi wa Huduma ya malipo ya ada ya Pasipoti kwa njia ya Airtel Money





Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhamiaji (SACI) Mohamed Awesu (kulia) ambae pia ndie Mfawidhi Mkuu wa TEHAMA Katika Jeshi la Uhamiaji Tanzania akitoa salamu ya kuagana na Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji Dorah Luoga (kushoto) ambae pia ndie Mdhibiti wa Pasipoti Katika Jeshi la Uhamiaji Tanzania baada ya kumaliza tukio la uzinduzi wa malipo ya Ada ya Pasipoti kwa njia ya Airtel Money


Uhamiaji Tanzania Jazz Band nayo haikubaki Nyuma ilisindikiza Tukio hilo kwa kutoa Burudani kabambe kwa wateja walihudhuria tukio hilo

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni