Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dkt. A. P.
Makakala ametoa salaam za Heri ya Sikukuu ya Uhuru wa Tanzania bara kwa Watanzania
alipokuwa akiwaaga watumishi wa Idara ya Uhamiaji Makao Makuu akielekea Mkoani
Dodoma kuhudhuria maadhimisho ya miaka 56 ya Uhuru wa Tanzania bara.
Akizungumza Ofisini kwake Kamishna huyo amewataka
Watanzania kudumisha uzalendo kwa kulinda Rasilimali, Ulinzi na Usalama wa nchi
kwa faida ya kizazi kilichopo na kijacho. Hii ikiwa ndio njia pekee ya kuwaenzi
waasisi wa Taifa letu.
“Uraia wetu una umuhimu wa kipekee kwani
umebaki kuwa ndio msingi na utambulisho wetu unaotaunganisha wananchi wote bila
ya ubaguzi ukilinganisha na utambulisho mwingine kama ukabila au dini na ndio
utambulisho wetu kimataifa.Taifa lolote huru liwe kubwa au dogo haliwezi
kukamilika bila ya kuwa na raia wake, ndiyo maana miaka 56 ya Uhuru wetu
tunajitambua na kujivunia kuwa Watanzania” Alisema Kamishna
Jenerali wa Uhamiaji.
Kwa msingi huo suala la kutambua nani ni raia
na nani ni mgeni litabakia kuwa lengo kuu la Idara, kwakuwa raia ndiyo
wanaotakiwa kunufaika na Rasilimali za nchi na Haki zinazotolewa na nchi kwa
raia wake.
Pamoja na haki hizo za Kikatiba na za asili,
lakini pia ni raia hao wenye wajibu wa kulinda Taifa lao dhidi ya uvamizi
wowote na rasilimali za Taifa kama zilivyopiganiwa na Mwasisi na Baba wa
Taifa letu Hayati Mwl Julius K. Nyerere na kuongeza kuwa jukumu la ulinzi na
usalama wa nchi ni la wananchi wote na hasa wazalendo.
Ni vyema kufahamu kuwa Uraia wetu ndio
Utanzania wetu hivyo basi hatuna budi kuadhimisha siku hii adhimu tukiwa
na ndoto na matarajio ya kuijenga Tanzania mpya ya Viwanda.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni